KILIMO BORA CHA UFUTA


KILIMO BORA CHA UFUTA
KILIMO BORA CHA UFUTA
KILIMO BORA CHA UFUTA: Ufuta ni zao linalolimwa kwa wingi katika mikoa ya Lindi, Mtwara, Ruvuma, Pwani, Morogoro, Dodoma, Tanga na ukanda wa chini katika mikoa ya Rukwa na Mbeya. Zao hili hulimwa kwa ajili ya chakula na biashara. Mbegu za zao hili huwa na wastani wa mafuta kiasi cha asilimia 45.

MAMBO YA KUZINGATIA WA KATI WA KUZALISHA MBEGU 
  1. Chagua aina ya mbegu inayotoa mazao mengi na bora, inayovumilia mashambulizi  ya magonjwa na wadudu, inayokomaa mapema na kutoa mafuta mengi.

  1. Chagua mbegu inayokomaa kwa pamoja ili kurahisisha uvunaji na pia kuepuka upotevu wa zao shambani.

  1. Aina nyeupe ya mbegu ya ufuta hupendelewa zaidi kuliko aina nyeusi.

UPANDAJI
Panda mbegu nusu inchi chini ya udongo, inchi sita umbali wa mbegu na mbegu na futi mbili nafasi ya msitari na msitari, kabla ya kupanda hakikisha ardhi imelowana vya kutosha na upande mbegu masaa mawili au matatu baadae

MBOLEA
Ufuta unahitaji rutuba ya kutosha ili kutoa mazao bora. Katika kudumisha rutuba ya udongo, tumia kilimo cha mzunguko wa mazao au weka mbolea za asili pale inapobidi.

PALIZI
Dhibiti magugu kwa kupalilia ili kuruhusu ufuta kutumia vizuri unyevu na virutubishi. Magugu mengine huwa ni maficho ya wadudu waharibifu wa zao la ufuta.

MAGONJWA NA WADUDU
Ufuta hushambuliwa na magonjwa na wadudu mbalimbali ambao huweza kusababisha upungufu na ubora wa mazao. Hivyo kagua shamba mara kwa mara hasa kwenye maua na mapodo ili kuona dalili za mashambulizi. Endapo kuna dalili zamashambulizi, chukua tahadhari mapema kabla ya uharibifu mkubwa haujatokea.

MAANDALIZI KABLA YA KUVUNA 
  1. Kagua shamba kuona kama ufuta umekomaa,  Ufuta hukomaa, kati ya miezi mitatu na   minne tangu kupanda kutegemea aina.
  2. Aina ya ufuta usiokuwa na matawi hukomaa mapema kuliko ile yenye matawi.
  3. Ni muhimu kuwahi kuvuna ili kuepuka ufuta kupukutikia shambani.

 DALILI ZA KUKOMAA UFUTA SHAMBANI
  • Kwa kawaida majani hubadilika rangi kutoka kijani na kuwa ya manjano na hatimaye kudondoka.
  • Mashina hubadilika rangi kutoka kijani na kuwa ya kahawia.

VIFAA VYA KUVUNIA
  • Kamba
  • Siko
  • Panga

VIFAA VYA KUKAUSHIA
  • Sehemu ya kukaushia yenye Sakafu ya saruji
  • Maturubai
  • Sakafu safi
 
KUVUNA
  1. Vuna ufuta mapema kabla mapodo kukomaa sana na kuanza kupasuka na kuachia punje.Mapodo ya ufuta yaliyokomaa sana yakiguswa au kutikiswa na upepo hupasuka na kuachia mbegu, hali inayosababisha upotevu mkubwa.

  1. Mbegu za ufuta ni ndogo na zikidondoka chini ni vigumu kuziokota. Vilevile mbegu zilizodondoka ni vigumu kuzitenganisha na uchafu.

  1. Kwa aina za ufuta zenye mapodo yanayopasuka, uvunaji ufanyike wakati mimea bado ni kijani ili kuepuka upotevu wa mbegu.

  1. Aidha uvunaji ufanyike wakati hakuna upepo wala jua kali.

  1. Baada ya kukata mashina yafunge katika mizigo midogo na kuweka katika vyombo vya kusafirisha kama vile mikokoteni, matela au magari hadi sehemu ya kukaushia.

  1. Panga mizigo midogo kwa kusimamisha katika malundo madogo yasiyozidi mizigo minane kwenye sehemu safi za kukaushia.

KUKAUSHA
Mapodo ya ufuta hukaushwa yakiwa yamefungwa katika vitita. Vitita huwekwa kwa kuegeshwa kwenye fremu ya kukaushia kwa muda wa wiki mbili hadi tatu kutegemea hali ya hewa. Fremu hii huwekwa juu ya turubai au sakafu ili kuzuia upotevu wa punje kutokana na kupasuka kwa mapodo.

KUPURA
Upuraji hufanyika kwenye turubai, mkeka au kwenye sakafu safi.
  • Vitita hupigwa taratibu kwa kutumia mti au hutikiswa vikiwa vimegeuzwa vichwa chini ili kuruhusu punje za ufuta kudondoka kwenye sakafu safi au turubai.

KUPEPETA NA KUPEMBUA
Kupepeta na kupembua hufanywa ili kuondoa takataka kama vile mawe, vipande vya mapodo,vijiti na vumbi. Njia bora ya kupepeta na kupembua ni kwa kutumia mikono.
Ufuta huwekwa kwenye vyombo kama vile ungo kwa kiasi cha kilo mbili hadi tatu. Ufuta hurushwa hewani kwa kasi ndogo na takataka nyepesi huchukuliwa na upepo. Zile nzito huondolewa kwa mikono.

KUFUNGASHA
Mbegu za ufuta zilizo safi huwekwa kwenye vifungashio kama vile magunia madogo ya aina ya juti ya ujazo wa kilo 50. Fungasha mbegu za ufuta kwenye magunia yenye uzito usiozidi kilo 50. Kabla ya kufungasha hakikisha mbegu zimekauka hadi kufikia unyevu wa asilimia 10.

  KUHIFADHI
  • Panga magunia ya ufuta juu ya chaga.
  • Panga kwa kupishanisha ili kuruhusu mzunguko wa hewa kati ya magunia.

KUSINDIKA MBEGU ZA UFUTA
Ufuta husindikwa kupata bidhaa ya mafuta ambayo hutumika katika mapishi mbalimbali. Mafuta hukamuliwa kwa kutumia njia za asili na kwa kutumia mashine. Njia za asili zina ufanisi mdogo ukilinganisha na zile za kukamua kwa mashine, hivyo ni vyema kutumia mashine. Kuna mashine za aina mbili zinazotumika kukamua mafuta; mashine za mkono na zile zinazoendeshwa kwa injini au mota ya umeme. Mashine za mikono zinazotumika zaidi hapa nchini ni za aina ya daraja (Bridge press) na Ram.

MATUMIZI
Mafuta ya ufuta hutumika katika mapishi mbalimbali ili kuongeza ladha. Pia husaidia kuleta nguvu na joto mwilini. Mbegu za ufuta huchanganywa na vyakula mbali mbali kama mikate, keki, mboga na kadhalika

Comments

Post a Comment

Popular Posts